SAID NASSORO MWAMBA “KIZOTA”
Buriani Said Nassoro Mwamba “Kizota” mtambo wa magoli na Nyota ya Magharibi iliyozimika ghafla.
NI MIAKA 10 imepita sasa lakini nakumbuka ni kama tuliko lililotokea jana.
ilikuwa tarehe 11 February, 2007 majira ya saa nne usiku nilipata ujumbe mfupi wa simu kutoka kwa Swedy Mwinyi wa Radio Tanzania, “.. salaam, Said Mwamba amefariki dunia kwa kugongwa na gari wakati anatoka Taifa!! Maiti ipo Mortuary Temeke..” Taarifa hii ya msiba, tena ya mtu unayemfahamu lazima imshitue mtu. Nilishituka sana baadaye nikamshukuru Mungu. Nilipigia simu mmoja wa Jamaa na rafiki wa karibu wa marehemu Said, Mchezaji wa zamani wa Simba na Yanga Kureish Ufunguo ambaye muda mfupi uliopita nilikuwa namtania kuhusu matokeo ya mechi ya Simba ya jana. Naye alishituka sana, masikini, naye hakuwa na taarifa akaniambia labda tumuulize Isack Gamba wa Radio One, nilipompigia akasema ni kweli!!. Ndivyo yalivyo maisha ya mwanadamu hapa duniani, kama Ua huchanua na kusinyaa.
Kwa mtu yeyote aliyemfahamu marehemu Said, atakiri na kukubaliana nami kuwa Taifa limepoteza mmoja wa mashujaa wake aliyelipigania Taifa lake katika medani ya Soka enzi za uhai wake. Alikuwa na kipaji cha ajabu katika soka na aliufanya mpira jinsi alivyotaka yeye.
Marehemu Said Mwamba alizaliwa na kukulia mjini Tabora kabla ya kuja Dar es Salam miaka ya 1980 katikati ambapo baadaye alijiunga na Dar es Salaam Youngs Africa (YANGA). Ameifanyia mengi Klabu hii ya Jangwani ambayo licha ya kuwa mchezaji alikuwa ni mdau wake mkubwa.
Kwa kipindi cha takribani miongo mitatu iliyopita Tabora ilikuwa ni mji uliotoa wachazaji wengi wenye vipaji tangia enzi za Gosaji Cup miaka ya 1960 kama Yunge mwana Sali, Hasan Rajab, Mzee kitenge na wengineo. Miaka ya 1970 kukawa na timu imara kama Sungura, Coastal, baadaye Tumbaku, Tindo, na Vita iliyokuwa Timu ya Jeshi enzi za Meja Jenerali mstaafu Mayunga alipokuwa mkuu wa Brigedi ya Magharibi.
Wakati marehemu Said anaanza kucheza mpira yeye na ndugu zake kina Rajabu na Ally Mwamba, kina Ufunguo na Abas Mchemba tayari Tabora imelishawahi kutoa wachezaji wenye vipaji walioliwakilisha Taifa kama kina Amasha, Athumani Maulidi-Big man, Hamis Kinye, marehemu Athumani Mambosasa, Rajab Risasi, Abdallah Mwinyimkuu pele ambao walimsawishi marehemu Said kuongeza bidii.
walikuwepo pia watu waliosomea shule za Tabora kama Daudi Salum Bruce Lee na marehemu Ibrahim Marekano Regan ambao walipata mafanikio makubwa na kuchezea timu ya wekundu wa Msimbazi Simba ziku za nyuma. Tabora ilikuwa na kituo cha kuibua vipaji vya watoto wadogo cha kanisa katoliki Tabora kilichokuwa chini ya ulezi wa father Damiano cha Chipukizi.
Ndani ya uwanja marehemu Said alikuwa na uwezo wa kucheza karibu namba zote. Alipotoka Tabora na kujiunga Yanga alikuwa anacheza nafasi ya kiungo mkabaji. Baadaye waalimu kama sikosei ni marehemu Tarzan alimbadili na kumfanya acheze kama mshambuliaji wa kati. Kuna wakati nilimuuliza sababu gani ilimfanya aende Simba kabla ya kuridi tena Yanga, akatabasamu na kuniambia kuwa mpira una mambo mengi.
Said alikuwa na uwezo mkubwa wa kupiga chenga tena za maudhi halafu anaukanyaga mpira na kuwaangalia wachezaji wa timu pinzani kama anayeuliza maswali? Kutokana na uwezo wake wa kumiliki mpira alifananishwa na jinsi marehemu baba wa Taifa alivyokuwa anaendesha vikao vya Chama kule kizota alipokuwa akiuliza maswali? Huku wajumbe wakisema hakunaa.
Wapenzi wa kandanda watakubaliana nami kuwa marehemu Said alikuwa na kipaji kikubwa. Mwaka 1993 alikuwa ni miongoni mwa wachezaji walioiwezesha Yanga kuutwaa Ubingwa wa Afrika ya Mashariki. Enzi hizo walikuwapo kina keneth Mkapa, Nemes, Mohammed Hussein Mmachinga, Abubakar Salum, Mwanamtwa Kihwelo, Zamoyoni Mogella, Edbily Lunyamila, marehemu Steven Mussa, Gagarino, marehemu Method Mogella na marehemu Riffat Said.
Marehemu Said Mwamba, mbali ya mafanikio aliyopata ndani ya uwanja, nje ya uwanja aliuweka kando u-super star wake, hakuwa mtu wa kujidai, alikuwa hawezi kumpita mtu aliyemfahamu bila kusimama na kumsalimia. Kuna habari ambazo sikuwahi kumuuliza marehemu said kama kweli alishawahi kuukataa uraia wa moja ya nchi za kiarabu (Abudhabi) ili aendelee kuchezea Yanga.
Wapo wachezaji ambao hata wenzao wanawakubali. Said ni mmoja wa wachezaji ambao hata wa Timu ya Taifa mwaka 2000 wakati tunajiaanda kucheza na Ghana wachezaji wenzake walimtaka kocha mkuu wa timu ya Taifa Mjerumani Bukhard Pape awaite kikosini Kizota na Masatu ili achwe huru kama wanamfaa
Nilipomuuliza kama kuna Timu nyingine aliyowahi kuipenda kama Yanga, marehemu Said alisema kuwa alikuwa anapenda sana uchezaji wa Timu ya Pamba wana kawe kamo enzi hizo ilipokuwa kwenye kiwango.
Taifa na wapenzi wa mpira hasa wa Yanga wamepata msiba mkubwa na vivyo hivyo kwa hata kwa wapenzi na wanachama wa Simba ambao marehemu alipata kuchezea. Kwa hali yeyote iwayo msiba huu ni mkubwa sana Tabora kwa sababu mji huo umepoteza mmoja wa watoto wake wenye vipaji vikubwa iliyopata kuwazaa. Wapo wachezaji wengi lakini alikuwapo Said Mwamba kizota mmoja na pengine itachukuwa miongo kadhaa kumpata wa mithili yake.
Wapo wachezaji wengi lakini alikuwepo Said Mwamba Kizoto Mmoja tu Tanzania.Buriani Said Mwamba kizota umetangulia kule ambako sisi tuliobaki tutakufuta. Wote tumetoka kwa Mwenyezi Mungu na kwake tutarejea.